Kamati ya bunge ya hesabu za serikali PAC imebaini upotevu wa fedha 
zaidi ya shilingi bilioni 1.5 za mamlaka ya usimamizi wa bandari TPA 
ambazo zimetumika lakini nyaraka zake hazionekani huku ikiuagiza uongozi
 wa mamlaka hiyo kuhakikisha fedha zote za nyongeza ya posho za safari 
walizolipwa watumishi tangu mwaka 2011 kabla msajili wa hazina 
hajathibitisha zinarudishwa.
Mwenyekiti wa kamati ya PAC Mh Zitto Kabwe ametoa agizo hilo wakati
 kamati yake ilipokutana na bodi na uongozi wa TPA baada ya kukagua 
vitabu vyake vya mahesabu ambapo amesema licha ya kiwango cha posho 
zilizolipwa kuwa kikubwa lakini waliharakisha kujilipa kabla msajili wa 
hazina hajathibitisha ambapo afisa wa ngazi ya juu alilipwa shilingi 
laki tano kwa siku kwa safari ya ndani ya nchi na ya nje ya nchi dola za
 kimarekani mia nane.
Akizungumzia suala la ukosefu wa nyaraka za fedha ambazo tayari 
zimeshatumika makamu mwenyekiti wa PAS Mh.Deo Philikonjombe amesema 
tatizo hilo limekuwa sugu kwa taasisi mbalimbali za serikali hali 
inayoashiria kuwa kuna baadhi ya wakurugenzi na watumishi wanafuja fedha
 za umma kinyume na taratibu na wanapobanwa wanapeleka nyaraka ambazo 
wakati mwingine ni za kufoji.
Kaimu mkurugenzi mkuu wa TPA na mhasibu wake mbali na kukiri 
upotevu wa nyaraka hizo wamedai kuwa tatizo hilo limetokana na uhifadhi 
wa nyaraka ambao hadi leo nyaraka nyingi za TPA zinahifadhiwa kwenye 
karatasi na kuiahidi kamati hiyo kuwa wataziwasilisha mwisho wa mwezi wa
 mwezi febuari mwaka huu hali iliyozua maswali mengi kwa wajumbe wa 
kamati hiyo kuwa watazipata wapi kama kipindi chote hicho hazijaonekana.

0 comments so far,add yours