HALI ya taharuki imetanda baada ya usiku mzima wa kuamkia jana Kikosi Maalumu cha Jeshi la Polisi cha Kupambana na Uhalifu, kupambana na genge la watu wanaosadikiwa kuwa majambazi au magaidi katika nyumba waliyokuwa wakiishi eneo la Vikindu, wilayani Mkuranga, Mkoa wa Pwani.
Katika mapambano hayo ambayo msingi wake ni operesheni ya kuwasaka watu walioua askari wanne wiki hii, inadaiwa Kamanda wa Kikosi Maalumu cha Kuzuia Uhalifu, Kanda Maalumu ya Dar es Saalam, Thomas Mniko, aliuawa.
Mniko anadaiwa kupigwa risasi na watu hao wanaodaiwa kuwa na utaalamu wa kutumia silaha nzito chini ya kiongozi wao anayedaiwa kuwa ni Luteni Kanali mstaafu wa Jeshi la Wananchi aliyepata mafunzo ya udunguaji nchini Cuba.
Wakati taarifa nyingine zikieleza kuwa Kamanda Mniko aliuawa kwa kupigwa risasi kifuani, nyingine zilikuwa zikieleza kichwani.
Mbali na kifo cha Mniko, kumekuwepo na taarifa tofauti ambazo hazijathibitishwa juu ya idadi ya watu waliouawa katika tukio hilo.
Wakati taarifa toka ndani ya Jeshi la Polisi zikidai kuwa waliouawa ni 14 huku tisa kati yao wanawake watatu wakishikiliwa na jeshi hilo, taarifa toka kwa viongozi wa eneo la Vikindu zilieleza waliouawa ni wawili.
Kutokana na uzito wa tukio lenyewe, Jeshi la Polisi liliamua kutotoa taarifa yoyote jana na kuahidi kufanya hivyo leo.
MTANZANIA JUMAMOSI LATUA VIKINDU
Gazeti hili lilifika eneo la tukio jana asubuhi na kushuhudia hali ya taharuki ikiwa imetanda huku askari wengi wakiwa wamezingira nyumba hiyo na zaidi wakizuia wananchi na waandishi wa habari umbali wa mita kama 100 kutoisogelea.
Wakizungumza katika eneo la tukio, baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo walisema walianza kusikia majibishano ya risasi toka katika nyumba hiyo iliyokuwa na wapangaji tangu saa 8 usiku wa kuamkia jana.
Kwa mujibu wa mashuhuda hao milio ya risasi ilikoma jana asubuhi saa 2:30.
Idadi ya watu waliokuwa wakiishi katika nyumba hiyo bado haijajulikana na kumekuwa na taarifa tofauti ambapo wapo wanaodai walikuwa wakiishi watu saba ambao ni baba, mke na watoto huku wengine wakidai ni familia mbili tofauti ambazo zilikuwa hazifahamiki.

KAULI YA OFISA MTENDAJI
Akizungumza na gazeti hili Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Vikindu, Abass Ndambe, alisema alianza kusikia majibizano ya risasi tangu saa 8 usiku ambapo aliamua kuwaamsha majirani zake ili kujua tatizo.
“Operesheni imeanza saa 8 usiku, tulisikia mlipuko lakini hatukujua dhahiri kama ni bomu au risasi za kawaida hapo tukaamshana, lakini hatukuweza kufika eneo hilo hivyo tulisubiri hadi asubuhi ambapo tulitaka kufika ili kujua kulikoni lakini askari walituzuia,” alisema Ndambe.
Ndambe aliyasema hayo baada ya kuitwa na kupewa taarifa juu ya tukio hilo na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Boniveture Mushongi.
Ndambe alisema RPC huyo alimweleza kuwa walikuja kumkamata mtuhumiwa wa mauaji ya polisi wanne yaliyotokea wiki hii eneo la Mbande, Temeke jijini Dar es Salaam baada ya wenzake waliokamatwa kumtaja.
“Katika majibizano ya risasi, RPC alisema watu wawili ambao ni askari mmoja na mtuhumiwa mmoja waliuawa. Hata hivyo, sijapata idadi ya waliokamatwa. Sijawahi kuona uhalifu mkubwa vile Vikindu ingawa kulikuwa na matukio ya uvunjaji wa maduka lakini si kwa majibizano ya risasi kama hivyo,” alisema Ndambe.
Akisimulia kilichotokea Mwenyekiti wa Mtaa huo wa Vikindu Mashariki, Mohammed Maundu, alisema usiku wa tukio saa 8, walifika askari ambao hakuweza kujua idadi yao wakiongozwa na Kamanda Thomas.
“Askari walifika na kugonga mlango wa nyumba waliyokuwa wakiishi watuhumiwa ambapo hapo hapo askari mmoja akapigwa risasi ya kifuani na kufa palepale. Baada ya kifo cha askari huyo kulitokea taharuki kwa askari ndipo yakaanza majibizano ya risasi hadi saa mbili asubuhi ambapo wamefanikiwa kuwakamata watu saba wa familia moja wakiwemo watoto waliokuwa ndani ya nyumba hiyo,” alisema Maundu.
Maundu alisema taarifa alizozipata zilidai kuwa hakukuwa na silaha iliyokamatwa jambo linaloonyesha kuwa aliyefyatua risasi iliyomuua askari huenda alikimbia.
“Waliokamatwa wamechukuliwa na askari kwa ajili ya kutoa maelezo zaidi, hivyo katika tukio zima hakuna mtuhumiwa aliyefariki,” alidai Maundu.
Alisema nyumba hiyo walikuwa wakiishi familia moja ambayo walikuwa ni wapangaji huku nje kukiwa na fremu za maduka.
“Mimi mwenyewe sikuwahi kujua kama katika nyumba hiyo kulikuwa na watu wanaishi tofauti na wafanyabiashara wenye fremu hapa nje.
Hakuna aliyewajua watu hawa kwa kuwa walikuwa wanaishi ndani bila kutoka nje na hata baba wa familia inaonekana alikuwa akitoka alfajiri na kurudi usiku mkubwa,” alisema Maundu.

VYANZO VYA POLISI
Wakati kukiwa na taarifa hizo, vyanzo vyetu vya habari toka ndani ya Jeshi la Polisi vilidai kuwa msingi wa tukio la jana ni operesheni iliyoanzishwa na jeshi hilo kwa ajili ya kuwasaka watu waliohusika na tukio la kuuawa polisi wanne wiki hii.
“Tulianza jana (juzi) saa mbili usiku kufanya operesheni hii ambapo tulifanikiwa kuwakamata wengine, katika mahojiano walituelekeza kuwa mkufunzi wao yuko Vikindu ndipo tukaelekea huko na katika mapambano watu wawili ambao ni askari na raia walifariki dunia huku wengine wengi wakitiwa nguvuni,” kilisema chanzo hicho.
Chanzo hicho kilidai mtuhumiwa aliyeuawa alikuwa amejificha kwenye dari ya nyumba hivyo baada ya kumtaka kuteremka na kushindwa kutii amri walimtungua huko huko kwa kumpiga risasi.
Akisimulia namna Kamanda Thomas alivyouawa chanzo hicho kilidai; askari walipofika eneo la tukio waliamuru watu hao kufungua mlango na kujisalimisha lakini walipogundua uwepo wa askari, watuhumiwa hao walifyatua risasi na ndipo majibizano yalipoanza na risasi ya kichwa kumpata Kamanda Thomas ambaye alifariki dunia papo hapo.
Chanzo kingine kutoka ndani ya Jeshi hilo kilidai kuwa baada ya tukio la kuuawa askari huyo, wenzake walivunja mlango na kuanza kumimina risasi ambapo walifanikiwa kuwaua watu 14 na kuwakamata wengine watano wakiwemo wanawake wawili.
Taarifa hizo zinashabihiana na zilizotolewa na chanzo kingine kutoka jeshi hilo ambacho kilidai kuwa katika eneo la mapambano waliuawa watu 14, askari mmoja na wengine tisa walikamatwa.
MAZINGIRA YA NYUMBA
Gazeti hili liliweza kuifikia nyumba hiyo ambayo mbele ina fremu tatu za maduka na kuona ikiwa imetobolewa kwa risasi ukutani, madirishani na mlango ambao ulivunjwa.
Katika nyumba hiyo yenye uzio wa tofali zilionekana nguo zenye damu na nyingine zisizo na damu zikiwa zimesambazwa chini, vyombo hasa ndoo za maji zikiwa haziko katika mpangilio mzuri hali iliyoonyesha namna mapambano yalivyokuwa makali.
MAJIRANI
Majirani wa nyumba hiyo (majina tunayahifadhi) waliliambia MTANZANIA Jumamosi kuwa walishangaa kuona kuna familia inayoishi nyumba hiyo kwa kuwa ilikuwa kimya muda wote.
“Mimi nimeshangaa kuona kuna watu wanaishi pale mie siwajui, nadhani walizuiwa kutoka ndani wakawa wanashinda uani kwao,” alisema.
Jirani mwingine, Hussein Mbando, alisema risasi zilipoanza usiku huo wa manane iliwalazimu kukesha hadi asubuhi.
“Hatujawahi kujua kama kuna watu hatari katika eneo hili kwa kuwa hawa watu walikuwa wakiingia usiku na kutoka usiku huku wake zao wakiwa hawatoki nje hivyo hatuwajui kabisa,” alisema Mbando.
MAKAMANDA WATUPIANA MPIRA
Tofauti na matukio mengine ambapo Jeshi la Polisi hutoa taarifa zake mapema, jana Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam ambaye naye alikuwa katika eneo la tukio alikataa kuzungumza chochote na kuahidi kutoa taarifa kamili leo.
Awali gazeti hili lilipomtafuta Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, RPC Mushongi, aligoma kuzungumza na kudai kuwa mtu anayepaswa kuzungumzia suala hilo ni Kamanda Sirro kutokana na askari waliohusika kutoka kikosi maalumu.
“Naomba muwasiliane na Kamishna Sirro ndiye anayeweza kutoa taarifa kwa sasa, ufafanuzi na maelezo zaidi,” alisema Kamanda Mushongi.
Naye Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Advera Bulimba, alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo alisema atafutwe Kamanda wa Polisi Temeke au Kamishna Sirro.
Gazeti hili pia lilimtafuta kwa njia ya simu Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Ernest Mangu ambaye alisema yupo kwenye kikao.

HALI ENEO LA TUKIO
Katika eneo la tukio ambalo gazeti hili lilipiga kambi tangu asubuhi lilishuhudia magari ya polisi zaidi ya 10 pamoja na mengine ambayo yalikuwa na namba binafsi.
Magari hayo yalikuwa ni pamoja na gari yenye namba PT 1860, PT 3612, gari ya RPC wa Pwani, magari mawili ya Jeshi la Zimamoto, gari ya maji ya kuwasha, gari la zimamoto na mengine.
Ilipofika saa sita kasoro mchana gari lingine la polisi lenye namba PT 3789 lilifika eneo la tukio likiwa limebeba askari wengine waliokuwa na silaha.
Si hao tu gazeti hili pia lilishuhudia pia askari wa Jeshi la Wananchi (JWTZ) wakiwa eneo la tukio ambalo lilikuwa limezongwa na wananchi kutoka katika viunga mbalimbali vya Mkoa wa Pwani na Dar es Salaam.
Baadhi ya wananchi walidai kutoka Tegeta jijini Dar es Salaam ili kushuhudia kwa kuwa walichoka kuona taarifa kwenye magazeti na runinga.
Pamoja na hali ya usalama kuimarishwa katika eneo hilo la tukio, lakini ilipofika saa saba kasoro baadhi ya gari za polisi zilianza kupungua.
Gari moja lilibaki ili kuwasubiri Zimamoto ambao waliondoka baada ya dakika chache na kuwatangazia wananchi kuondoka eneo la tukio ili wakaendelee na shughuli zao za kila siku.
VIZUIZI NJIANI
Hali ya usalama barabarani ilikuwa imeimarishwa huku askari wa usalama wakiwa wametanda maeneo mbalimbali ya mkoa wa Pwani hadi Dar es Salaam.
Katika hali isiyokuwa ya kawaida licha ya kuzoeleka kuwepo kizuizi kimoja tu cha polisi eneo hilo ambacho kiko Vikindu, gazeti hili lilishuhudia kizuizi kipya eneo la Kongowe ambalo ni mpaka kati ya Dar es Salaam na Pwani.
Katika kizuizi hicho, askari walikuwa na kazi ya kukakuga kila gari lililokuwa likipita eneo hilo hali iliyosababisha foleni kuwa kubwa.
MATUKIO YA MAUAJI YA POLISI
Ndani ya kipindi cha miaka miwili sasa kumekuwa na mfululizo wa matukio ya kihalifu dhidi ya askari wa Jeshi la Polisi nchini, ambapo baadhi ya askari wameuawa na wengine kujeruhiwa na watu wanaosadikiwa kupata mafunzo maalumu ya kutumia silaha.
Uvamizi huo pia umekuwa ukiambatana na uporaji wa silaha aidha kwenye vituo vya polisi, kwenye malindo au katika doria.
Mfano wa matukio hayo ni hili lililotokea wiki hii la askari wanne kuuawa.
Majambazi hao baada ya kutekeleza mauaji hayo, walivamia Kituo cha Polisi cha Mbande kisha wakavunja stoo na kuchukua sare ya askari na silaha.
Katika mfululizo wa mashambulizi kama hayo, Septemba 7 mwaka 2014 huko wilayani Bukombe, polisi wawili waliuawa na bunduki 10 aina ya SMG kuporwa katika Kituo Kikuu cha Polisi cha Wilaya ya Bukombe mkoani Geita.
Katika tukio hilo mbali na kupora SMG 10, pia walipora risasi ambazo idadi yake haikufahamika pamoja na mabomu ya kurusha kwa mkono.
Juni 12, 2014 watu sita wakiwa na pikipiki tatu walivamia kituo kidogo cha Polisi cha Mkamba kilichopo Kimanzichana, Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani na kuua askari mmoja na mgambo wawili, kisha kupora bunduki na risasi 60.
Julai 12, 2015 kundi la watu kati ya 16 au 18, lilivamia Kituo cha Polisi cha Stakishari, Ukonga jijini Dar es Salaam na kuua askari wanne na raia watatu kisha yakapora silaha aina ya SMG 15 na simu moja ya upepo.
Januari 21, 2015 watu waliojihami kwa silaha walivamia Kituo cha Polisi cha Ikwiriri, Wilaya ya Rufiji mkoani Pwani na kuua askari wawili, kisha yakapora silaha zilizokuwapo kituoni hapo.
Silaha hizo zilizoporwa ni aina ya SMG mbili, SAG mbili, Shotgun moja pamoja na silaha mbili za mabomu ya machozi na risasi za SMG.
Januari 27, 2015 huko mkoani Tanga, watu waliodhaniwa kuwa ni majambazi walivamia na kujeruhi askari wawili waliokuwa doria na kuwanyang’anya silaha mbili aina ya SMG.
Bunduki hizo ni aina ya SMG zenye namba 14301230 na 14303545.
Februari 3, 2015 kundi la watu lilivamia Kituo Kidogo cha Polisi Mgeta, Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro na kuiba bunduki aina ya SMG ikiwa na risasi 30. Pia waliiba jenereta, redio, viti, betri ya gari na spika ya redio.
Machi 30, 2015, askari wawili waliuawa na mmoja kujeruhiwa na majambazi, huko Kongowe jijini Dar es Salaam kisha yakapora bunduki mbili aina ya SMG.
Mei 29, 2015 watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi, walimvamia kwenye lindo askari wa Kikosi cha Tazara jijini Dar es Salaam na kupora bunduki aina ya SMG.
Share To:
Magpress

MagPress

Vestibulum bibendum felis sit amet dolor auctor molestie. In dignissim eget nibh id dapibus. Fusce et suscipit orci. Aliquam sit amet urna lorem. Duis eu imperdiet nunc, non imperdiet libero.

0 comments so far,add yours